UPO mpasuko wa wazi ndani ya Chama cha Mapinduzi (CCM), kama ambavyo vikao na matamko mbalimbali yanayotoka kwenye chama hicho yanavyoonyesha, hasa kuhusu sakata la serikali kulipa mabilioni ya shilingi kwa kampuni ya Dowans.
Baada ya kauli ya Umoja wa Vijana wa CCM juzi kumtaka mwenyekiti wa chama hicho, Jakaya Kikwete, achukue maamuzi magumu kukinusuru chama, hasa kwa kuwachukulia hatua kali vigogo wawili, Waziri wa Ushrikiano wa Afrika Mashariki, Samuel Sitta, na Naibu Waziri wa Ujenzi, Dk. Harrison Mwakyembe, Kamati Kuu ya chama hicho imetoa tamko la onyo kwa vijana hao.
Katibu Mwenezi John Chiligati aliwaambia waandishi wa habari jijini Dar es Salaam ‘amri’ ya vijana hao kwa Rais Kikwete kwamba awachukulie hatua Sitta na Mwakyembe ni suala la serikali na si la chama.
Alisema kufanya hivyo ni kuingilia mamlaka ya Rais iliyowekwa kwa mujibu wa sheria ambayo hutumika kuongoza nchi na kwamba Kamati Kuu inaiachia serikali kuliangalia hilo.
Huku akisisitiza kwamba tamko la UVCCM ni haki ya kitengo hicho cha chama, alisema Kamati Kuu itawaelimisha zaidi vijana hao na akasisitiza: “Ni lazima maamuzi ya chama yaheshimiwe.”
Alisema maamuzi ya kikao cha Kamati Kuu iliyokutana Januari 20, mwaka huu, imejadili masuala mbalimbali ikiwemo hali ya siasa nchini na kusema kuwa ni lazima serikali iheshimu maamuzi ya mahakama ya kimataifa ya biashara kuhusu mgogoro wake na TANESCO, unaolazimu serikali kuilipa Dowans fidia ya sh 94 bilioni.
Alisema hukumu hiyo ni funzo tosha kwa serikali, hasa katika kuingia mikataba ya miradi ya maendeleo na hata inapotaka kuivunja ni lazima ifuate sheria zilizopo, ikiwa ni pamoja na kufanya makubaliano yenye tija kwa taifa.
“Tunajua hili lililotokea hasa kutokana hukumu ya TANESCO kwa Dowans, tunajua kila Mtanzania ana haki ya kutoa maoni lakini kubwa ni uamuzi wa kisheria na hatuna budi kuuheshimu; kwanza tusubiri uamuzi wa pingamizi lililowekwa Mahakama Kuu ndipo taratibu nyingine zifuatwe na hata tamko la UVCCM ni maoni yao tutakaa nao sisi kama chama na kuwaelekeza taratibu za chama, “ alisema Chiligati.
Alisema TANESCO ilifanya kosa, na Kamati Kuu inaisisitizia serikali umuhimu wa kuzingatia na kuheshimu sheria, ikiwamo maamuzi yaliyotolewa na Mahakama ya Kimataifa ya Biashara (ICC).
Hata hivyo, alisema pamoja na hukumu hiyo, ni vema serikali ikasubiri uamuzi wa mahakama kuhusu pingamizi lililofunguliwa na Kituo cha Sheria na Haki za Binaadamu (LHRC) juu ya malipo hayo.
Sakata ya Dowans
Chiligati, alisema Kamati Kuu imeona ni vema kuheshimu maamuzi ya Mahakama na hakuna budi kutekeleza hukumu hiyo ila ni busara kwa serikali kutolipa malipo hayo ya bilioni 94 hadi uamuzi wa Mahakama Kuu kuhusu pingamizi lililowekwa na Kituo cha Haki za Binaadamu liamuliwe ndipo taratibu nyingene zifuate kwa mujibu wa sheria.
Migomo ya Wanafunzi, Wahadhiri wa Vyuo Vikuu nchini
Alisema ni vema serikali ifuatilie kwa makini suala hilo na kulipatia ufumbuzi wa haraka na kama kuna tatizo la malipo ilitakiwa kulipwa kwa wahusika ili kuondokana na hali ya migomo ya kila mara.
Alisema ufuatiliaji wa karibu utasaidia kubaini matatizo na hata kupata suluhu ya kudumu kwa haraka na ikiwezekana kumaliza hali hiyo.
Ila ni muhimu kwa wanafunzi na wahadhiri kuwa na utaratibu wa kutoa matatizo yao kabla na kuacha utaratibu hadi mambo yanapoharibika.
Aidha alisema kukaa meza moja mara kwa mara baina ya serikali na wahadhiri kutasaidia kujadiliana kwa kina na kugundua matatizo na kuyapatia ufumbuzi kwa wakati.
Vurugu za Arusha
Katibu Mwenezi huyo wa CCM, alisema kamwe chama chake hakiko tayari kurudia uchaguzi wa Meya kwani uchaguzi ulifuata taratibu zote za kisheria mbali ya CHADEMA kususia uchaguzi huo.
Alisema katika tatizo hilo ni vizuri CHADEMA wakawa wakweli kwani waliweka pingamizi dhidi ya Mbunge wa Viti Maalum, Mary Chatanda na kusahau kuwa CCM ina wajumbe 16, huku wao wakiwa na wajumbe 14 na TLP mmoja.
Alisema kitendo kilichotokea Kamati Kuu imekijadili kwa kina na kusikitishwa na vurugu hizo zilizopelekea kupoteza maisha ya watu watatu na wengine kujeruhiwa kutokana na kadhia hiyo.
“Ni vizuri CHADEMA wakawa wakweli wamesahau Mbunge wa Viti Maalum hupangiwa eneo la kazi na chama chake, kama wao walivyofanya kwa wabunge wao wawili hali ya kuwa wanaishi Moshi mjini lakini wakapelekwa wilayani Hai na wakashiriki kupiga kura, sasa tatizo liko wapi mbona sisi hatujalalamika ila wao tu ndio wafanye hivyo!?” alisema Chiligati.
Maadhimisho ya miaka 34 ya CCM
Kada na kiongozi huyo wa CCM, alisema Febreuari 5, mwaka huu, CCM itatimiza miaka 34 ya kuzaliwa kwake ambapo sherehe za maadhimisho hayo zitazinduliwa jijini Dar es Salaam Februari Mosi, mwaka huu na Makamu Mwenyekiti wa CCM Zanzibar, Amani Abeid Karume.
Alisema kuwa katika maadhimisho hayo wameyataka matawi ya CCM nchi nzima kufanya mikutano mikuu na kufanya tathmini ya kina namna ya walivyoshinda uchaguzi na hata maeneo waliyoshidwa kuwa wakweli.
Alisema maadhimisho hayo yatakwenda sambamba na mikutano ya hadhara kwa nchi nzima kwa kuwashukuru wananchi kwa kuichagua CCM katika Uchaguzi Mkuu uliopita na Februari 5, kilele chake kufanyika mkoani Dodoma na kuhitimishwa na Rais Kikwete kwa kupokea maandamano ya mshikamano.
Semina kwa wabunge wa CCM
Alisema CCM itafanya semina kwa wabunge wake 260 leo katika Hoteli ya Blue Pearl Ubungo Plaza, jijini Dar es Salaam ili kuwapa uelewa wa namna ya Bunge na kanuni zake kwa mujibu wa sheria.
Alisema Uchaguzi uliopita zaidi ya asilimia 60 ya wabunge wake ni wapya na 40 ni wa zamani hivyo ugeni wao CCM imeona ni muhimu kuwafanyia mafunzo hayo ili kwenda sambamba na kasi na viwango vya wabunge wa Chama cha Mapinduzi.