Pages

BRAND NEW MUSIC

metty magese

metty magese

Listen & Download

http://mdundo.com/a/32626

Sunday, November 17, 2013

Tanzania yavunja kambi ya watoto wanaopata mafunzo ya al-Shabaab katika mkoa wa Tanga

Polisi wa Tanzania walivunja zoezi la mafunzo ya al-Shabaab katika mkoa wa Tanga, kuwakamata washukiwa 69 na kuwaachia huru dazani za wafundishwaji wakiwa na umri wa miaka kati ya 4 hadi 13 katika usafishaji wa usalama uliofanyika tarehe 28 Oktoba hadi tarehe 5 Novemba.
Watoto wadogo wenye umri wa miaka minne walikutwa wakitiwa kasumba na watu wenye tabia za al-Shabaab huko Tanga. Hapo juu ni vipande vya taarifa ya video iliyoandaliwa na chombo cha habari cha al-Kataib cha al-Shabaab, ikionyesha wavulana wadogo wakifundishwa huko Somalia.

"Hii imetushitua, tumeongeza usalama katika wilaya ya Kilindi na tumewasambaza polisi jamii wa kutosha ambao wanalijua eneo vizuri, na kupitia operesheni za pamoja na polisi wetu tunapaa majibu yanayotia moyo," Kamanda wa Polisi wa Mkoa wa Tanga Constantine Massawe aliiambia Sabahi, akihakikisha idadi ya waliokamatwa.

Siku ya kwanza ya operesheni, polisi waliwaachia watoto 54 na wanawake 32 ambao walikutwa katika kituo cha mafunzo huko Lwande na kuwaunganisha tena na familia zao katika wiki ya kwanza ya mwezi Novemba, kwa mujibu wa Mkuu wa Wilaya ya Kilindi Selemani Liwowa.

Kuzitia kasumba akili changa

Watoto wengine 20, wenye umri wa miaka kati ya 4 na 13 na ambao "wamefundishwa kikamilifu" na al-Shabaab katika msikiti wa wenyeji, walikuwa wamewekwa katika programu ya urekebishwaji, Liwowa aliiambia Sabahi.

Wakati polisi walipowakuta katika msikiti wa Madina, vijana hao walikuwa na madaftari yaliyokuwa na mafunzo ya "jinsi ya kuua kwa kutumia kisu [au] panga, jinsi ya kupambana na wabishi kwa kutumia silaha na bila [silaha], jinsi ya kuhujumu uchumi na jinsi ya kuikomboa Afrika Mashariki katika mikono ya makafiri [infidels]," kwa mujibu wa Liwowa.

Al-Shabaab waliwafundisha watoto hawa katika kiwango kwamba walijitoa kwa wazazi wao kama sio Waislamu wa Kweli kwa sababu wanashirikiana na wasiokuwa Waislamu, alisema.

  Wakati wa msako katika msikiti huo, polisi pia walikamata mikanda ya video 12 yenye mafunzo ya al-Shabaab ya jinsi ya kuwakomboa Waislamu Afrika Mashariki na dunia kwa ujumla, alisema.
Kiongozi wa kikundi, mwenye jina la Ayubu na anayejulikana kama "Master", alikimbia dakika chache kabla ya kuwasili kwa polisi msikitini, lakini walimkamata msaidizi wake, mkaazi wa mkoa wa Singida aliyebainishwa kama Bw. Jumanne, alisema Liwowa.

Watoto walikabidhiwa kwa wafanyakazi wa kijamii kwa ajilii ya programu ya mabadiliko ya wiki tatu, alisema Mkuu wa Wilaya ya Tanga Halima Dendego. Kama wako tayari, watoto wataunganishwa tena na familia zao, alisema.
 
"Mshangao wangu ni jinsi watoto hawa wadogo wavyolikuja kukutana na wafundishaji hawa," Dendego aliiambia Sabahi. "Unamkuta mtoto wa miaka minne ambaye wazazi wake hawajulikani, na unashangaa ni jinsi gani walimshikilia mtoto mdogo kama huyu."

Wazazi wanahitaji kuelimishwa kuhusu umuhimu wa kuwapeleka watoto wao shule ili wasiangukie katika makundi ya kigaidi, alisema Dendego.

Kuongezeka kwa vitisho vya al-Shabaab?

Kuwepo kwa al-Shabaab wilayani humo kulitambulika ndani ya wiki ya mwisho ya mwezi Oktoba, wakati wananchi wasamaria wema walipowafahamisha viongozi wa serikali kuhusu kambi ya mafunzo iliyopo katika msitu wa Lwande.
"Tulipata taarifa kutoka kwa wasamalia wema, hususan wafugaji ambao mifugo yao ilikamatwa kila ilipokatiza jirani na kamba hiyo ya mafunzo," alisema Liwowa. "Pia, [wafundishaji wa al-Shabaab] walikuwa wakiwafukuza na kuwanyang'anya ardhi wenyeji kwa kiasi ambacho walipata ekari 500."
 
Viongozi wenyeji wamejifunza kwamba wafundishaji wanne wa al-Shabaab waliwasili katika wilaya ya Kilindi mwaka 2008 na kujiunga na msikiti wa Madina, lakini wanakijiji walijitenga na wafundishaji baada ya kuona mawazo yao yalikuwa na msimamo mkali, alisema Liwowa.

"Baada ya mapigano hayo mwishoni mwa mwaka 2008," yakitokana na mzozo uliotokea ndani ya msikiti kati ya wenyeji na wanachama wa al-Shabaab, "wafundishaji hao walinunua kipande chao cha ardhi na kujenga msikiti tofauti ambao sasa waliutumia kufundishia mafunzo ya al-Shabaab," alisema.

Kutokana na taarifa zilizokusanywa hadi sasa, baadhi ya watoto waliopata mafunzo kutoka kwa al-Shabaab katika wilaya ya Kilindi wamepelekwa Somalia kupitia Mombasa, Kenya, alisema Liwowa. Idadi kubwa ya wafundishaji wa al-Shabaab kutoka Somalia na Mombasa pia walikuja Kilindi mwanzoni mwa mwaka 2013, na inaonekana kuwa na mkakati wa ufundishaji katika mikoa mingine, kama vile Kilimanjaro, Zanzibar, Pwani na Mtwara.

Operesheni ya polisi katika wilaya ya Kilindi inafuatia ukamatwaji wa tarehe 7 Oktoba wa washukiwa 11 wa al-Shabaab waliokuwa wakifanya mafunzo ya kijeshi katika mkoa wa Mtwara.
Aidha, polisi walimkamata mfanyabiashara wa Tanzania Juma Abdallah Kheri tarehe 31 Oktoba huko Tanga kwa kushukiwa kwamba alikuwa akijihusisha na kuwaghiramia makundi ya kigaidi nchini Tanzania na washirika wa al-Shabaab nchini Kenya, Kituo cha Vijana Waislamu.

Alipoulizwa Tanzania inafanya nini kukabiliana na vitisho vya al-Shabaab vinavyoonekana kuongezeka, Mkurugenzi wa Uchunguzi wa Makosaya Jinai Robert Manumba alisema polisi walikuwa wakishirikiana na mashirika mengine ya usalama kupamaba na tatizo hilo.

"Tumeunganisha idara zote za usalama kuunda timu maalumu. Timu hiyo inahusisha maofisa usalama kutoka polisi, jeshi, huduma yetu ya upelelezi ya taifa, uhamiaji na [Mamlaka ya Mapato Tanzania] ambao wanafanya kazi kwa kushirikiana kutafuta suluhisho litakalodumu," Manumba aliiambia Sabahi.

No comments: